Tuesday, April 1, 2014

SERENA SEHEMU YA 1







          Ndege iliyombeba mzee Albano sostenes mwakatala ilipunguza kasi taratibu na hatimaye ikasimama.Tayari gari la wagonjwa lilikwisha fika na wauguzi na madaktari walikuwepo tayari kuhakikisha mzee Albano anapatiwa kila huduma inayohitajika wakati akishushwa toka ndegeni na kupelekwa hospitali kwa matibabu zaidi
.Kiongozi wa msafara ule wa madaktari na wauguzi toka hospitali kuu ya Patrick  memorial hospital Dr.Henry Mgumbwa alikuwa pembeni akibadilishana hili na lile na madaktari wenzake.
            Kutoka serikalini alikuwepo mheshimiwa waziri wa afya akiiwakilisha serikali ,pamoja na viongozi mbali mbali,vile vile walikuwepo viongozi wa dini toka madhehebu mbali mbali, na viongozi wa kisiasa pia walikuwepo.Ilimradi kila nyanja ambayo iliguswa na taarifa za kurejeshwa nchini mzee Albano ilituma mwakilishi wake.
            Familia ya mzee Albano ilishuka ndegeni ikiongozwa na mke wake na binti zake wawili Serena na Isabella wakiambatana na mmoja wa wafanyabiashara wakubwa nchini mzee Bryson Kamutere ambaye ni mshirika mkubwa wa kibiashara wa Albano Mwakatala aliyeambatana nao India ,wakasalimiana na kufarijiwa na ndugu na viongozi kadhaa wa serikali waliokuwa pale uwanjani pamoja na viongozi wa dini.Ilikuwa ni hali ya simanzi kubwa.Huko nje ya uwanja kulikuwa na umati mkubwa  wa watu na magari ambao wote walionyesha jinsi gani mzee Albano alivyokuwa mtu wao wa muhimu.
            Taratibu zote zikakamilika hapo uwanjani  kisha mzee Albano huku akiwa hana fahamu  ,akapakiwa katika gari la wagonjwa na safari ya kuelekea hospitali ikaanza.
            Taarifa za kurejeshwa nchini Mzee Albano Mwakatala zilisambaa karibu kila kona ya nchi.Magazeti yaliandika kwa kirefu juu ya kushindikana kupona huko nchini India na kisha madaktari bingwa kushauri arejeshwe nyumbani ,kwa sababu hakukuwa tena na tumaini  la kupona,kilichosubiriwa ni siku ya kufariki kwake.Madaktari katika hospitali kubwa nchini India walijitahidi kwa muda wa zaidi ya mwezi mmoja katika kujaribu kuutibu ugonjwa wa mzee Albano bila mafanikio.
            Mzee Albano alikuwa ni mmoja kati ya watu wenye heshima kubwa sana nchini Tanzania.Alikuwa mmoja kati ya wawekezaji wakubwa wazawa,aliyewekeza katika  viwanda vya kusindika mazao ya kilimo karibu kila mkoa na siku zote alikuwa akijitahidi na kuipigia kelele sana serikali juu ya kuongeza ajira kwa wazawa.Hii ilimfanya ajulikane na kupendwa .Pamoja na kuwa mmoja kati wa wawekezaji wakubwa nchini,ambaye alichangia kupatikana kwa ajira lukuki kupitia kampuni zake,alikuwa pia ni kimbilio kubwa kwa wale watu masikini wenye matatizo mbali mbali.Karibu kila mwezi alikuwa akilipia gharama za operesheni kubwa kubwa za watu mbali mbali wasiokuwa na uwezo,ndani na nje ya nchi achilia mbali kulipia gharama za elimu kwa watoto ambao wazazi wao hawakuwa na uwezo wa kuwasomesha,vile vile aliweza kuvisaidia vikundi vingi vya akina mama na vijana katika kujikwamua kimaisha.Ni mzee aliyekuwa na heshima ya pekee katika jamii ya watanzania.
            Albano Sostenes mwakatala ,ambaye baba yake alikuwa na asili ya Ureno alizaliwa mkoani Mbeya wakati huo baba yake akiwa mwekezaji mkubwa katika kilimo cha mpunga mkoani humo.Baba yake alioa mwanamke mweusi kutoka mkoani mbeya na wakafanikiwa kupata mtoto mmoja tu ambaye ndiye yeye mzee Albano.Alikulia mkoani Mbeya hadi alipomaliza elimu ya sekondari na kujiunga na chuo kikuu cha Kilimo ambako alihitimu shahada ya kilimo.Akaenda tena kuendelea na masomo nchini Japan katika kilimo cha Mpunga kwani alitaka kuendeleza kazi aliyokuwa akiifanya baba yake.Ni wakati huo ndipo alipopatwa na pigo kubwa la kuondokewa na wazazi wake wote wawili waliofariki kwa ajali ya gari.Alirudi nchini baada ya kumaliza masomo yake nchini Japan ,akaendeleza miradi ya kilimo aliyoiacha baba yake kwa ufanisi mkubwa. Ndani ya miaka miwili alikuwa amepiga hatua kubwa na kuongeza mtaji mara dufu ya ule wa baba yake.Hii ikamfanya ajikite tena zaidi katika uwekezaji mwingine.Akafungua viwanda karibu kila mkoa ili kuyaongezea thamani mazao ya wakulima.Akawa tegemeo kubwa la mazao ya wakulima nchini.Biashara yake ikawa kubwa sana na sasa akawa mmoja kati ya wawekezaji wakubwa na hapo ndipo alipoamua kuhamia mkoani Dar es salaam kwa sababu za kibiashara.
            Alioa mke wake aliyekuwa  mzaliwa wa Mbeya ambaye walikutana masomoni nchini Japan.wakafanikiwa kupata watoto wawili wa kike wenye uzuri usioelezeka Serena na Isabella.
             Siku moja akiwa katika safari zake za kibiashara alivamiwa na kundi la watu watu wenye silaha wanaosadikiwa kuwa ni majambazi ambao walimshambulia wakiwa na lengo la kumuua lakini kwa msaada mkubwa wa walinzi wake majambazi wale hawakufanikiwa kumuua badala yake walifanikiwa kumpiga na na kitu kizito kichwani na kumuacha akiwa hana fahamu.Tukio lile lilipelekea umoja wa wafanyabiashara kucuhukua maamuzi ya kumpeleka mzee Albano nje ya nchi kwa matibabu  ya haraka.Akiwa nchini India alikopelekwa kwa matibabu  alifanyiwa uchunguzi na jopo la madaktari bingwa  wakijaribu kutafuta namna ambayo wangeweza kufanya upasuaji .Hatimaye waliita familia yake na kuieleza ukweli kuwa operesheni hiyo ilikuwa ni haitawezekana kwa mzee Albano kufanyiwa upasuaji wa kichwa kwa sababu hakukuwa na tumaini la kupona hata kama angefanyiwa upasuaji huo.Taarifa hii ilikuwa ya mstuko mkubwa sana kwa familia yam zee Albano.Suala la kufariki baba yao lilikuwa ni msamiati mgumu kwa familia hii,hivyo wakataka kumuhamishia nchini Marekani katika hospitali kubwa zaidi,lakini mmoja wa wafanyabiashara wakubwa nchini mzee Bryson kamutere ambaye ni rafiki mkubwa wa Albano aliyeambatana na familia ya Albano nchini India akawashauri kwamba wazingatie ushauri wa madaktari wale bingwa na kurejea nyumbani kwani hata wangekwenda wapi hakukuwa tena na tumaini la mzee Albano kupona.Hatimaye baada ya majadilino marefu mke wa mzee Albano alikubali kumrejesha mumewe nchini kama alivyoshauriwa na madaktari.
            Kwa muda wa wiki nzima vyombo vya habari viliandika  kwa wingi taarifa za  mzee Albano.SIKU ZA ALBANO ZINAHESABIKA,KABURI LA ALBANO LAANDALIWA,TAIFA LAJIANDAA KUOMBOLEZA,hivi ni baadhi tu ya vichwa vya habari vilivyokuwa vikipamba magazeti ya kila siku,hali iliyoamsha wasi wasi mkubwa miongoni mwa wale waliomfahamu na kumpenda mzee Albano.
             HHHHatimaye siku ya kurudishwa nyumbani  mzee Albano ikawadia.Siku iliyokuwa na majonzi tele.Watu waliokuwa hapo uwanjani ni kama vile walikuwa msibani.Maongezi yalikuwa ni ya chini chini kila mmoja akionyesha huzuni aliyonayo.Pamoja na kuwa ni siku ya kazi lakini huwezi amini umati wa watu uliokusanyika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere.
            Patrick Charles memorial hospital ni moja kati ya hospitali kubwa kuwahi kujengwa nchini Tanzania.Ilikuwa ni hospitali ya aina yake kwa kuwa ilikuwa na uwezo wa kutibu karibu kila ugonjwa.Hospitali hii ilijengwa mahususi kwa ajili ya kumbukumbu ya Dr Patrick Charles mmoja kati ya madaktari waliojitolea maisha yao katika kuwasaidia watu masikini.Katika kuuenzi mchango wa baba yake ,Patrick Jr akaamua kujenga hospitali hii kubwa na ya aina yake ili kutoa matibabu kwa watu wote na hasa yale magonjwa makubwa yaliyoshindikana katika hospitali nyingine zote hivyo kupunguza gharama za kupeleka wagonjwa nje ya nchi kwa ajili ya upasuaji na matibabu.Hospitali hii iliyosheheni mabingwa wa kila fani ilihudumia si tu Tanzania bali hata nchi zote zinazoizunguka.
            Eneo lote la kuegesha  magari katika hospitali hii kubwa lilijaa magari kwa mara ya kwanza toka hospitali hii imefunguliwa.Watu wote hawa walikuwa wamekuja kuonyesha mshikamano wao kwa mzee Albano na kumtakia afya njema.Gari la wagonjwa lililombeba Mzee Albano likaingia hospitalini hapo,likaingizwa mpaka ndani kabisa na mzee albano akiwa bado hajitambui akapokelewa na kupelekwa katika chumba maalumu kwa ajili ya kupatiwa uangalizi .
            Kila kitu kilifanyika kwa haraka na kwa umakini wa aina yake.Dr Henry alikuwa bega kwa bega na madaktari wake kuhakikisha kuwa kila kitu kinakwenda kama kilivyopangwa.Baada ya kuhakikisha kila kitu kiko safi na tayari Mzee Albano anaendelea kupatiwa matibabu akaelekea ofisini kwake.Akabonyeza namba kadhaa katika simu yake ya mezani
            “Hallow Dr Henry hapa toka Patrick Charles memorial hospital,Naomba kuongea na Dr Jason tafadhali” Akasema Dr Henry
            “ Dr jason hawezi kuongea nawe muda huu yuko katika upasuaji.Baada ya kama dakika kumi hivi atakuwa amemaliza”
             “Ok akimaliza upasuaji tafadhali naomba anipigie ni muhimu mno”
            Dr Henry akakata simu kisha akapiga simu mapokezi na kuomba mke wa Mzee Albano na wanae waweze kupandisha ofisini kwake.
            “Karibuni sana .” Akasema Dr Henry baada ya mke wa mzee Albano na wanae kuwasili ofisini
             “Kwanza napenda kuwapa pole nyingi sana kwa kazi kubwa mliyoifanya ya kumuuguza mzee wetu mpaka katika hatua hii aliyofikia .Mama na wanao mnastahili pongezi kwa ujasiri mkubwa mliouonyesha.Papo hapo bado tunazidi kuwaomba mzidi kuwa wavumilivu kwa sababu hali ya mzee wetu bado si nzuri sana kama wenyewe mnavyoona na kwa mujibu wa taarifa za kidaktari.Sisi hapa tunaahidi kufanya kila tunaloweza ili kumpa tiba inayostahili mzee wetu mpaka hapo baadae kwani tumepokea taarifa toka kwa mheshimiwa rais kwamba tufanye kila linalowezekana kumsaidia mzee Albano. Tunaye Daktari wetu bingwa wa mambo ya mishipa ya fahamu ya ubongo na uti wa mgongo,kwa sasa yuko Dodoma kikazi ,nimempigia simu sasa hivi lakini  bado yuko katika upasuaji hivyo muda wowote atapiga simu atakapomaliza .Nataka naye arudi mara moja leo hii hii ili aongoze jopo la madaktari katika kumpa tiba mzee wetu.Ninamuamini Dr Jason ni daktari wa ian yake hapa nchini na nina hakika baada ya kumuona na kumfanyia uchunguzi mzee wetu basi anaweza akatupa uhakika kama atapona au hatapoa.Kwa sasa msiwe na wasi wasi sana kwani hata kama huko Nje ya nchi wameshindwa sisi hatuwezi kukata tamaa kirahisi kwani si mara moja kuna watu wameshindikana kupona huko nje ya nchi lakini wamekuja kupona hapa.…….”kabla hajaendelea simu ikaita akaipokea
            “Hallow,Dr Henry hapa”
            “Dr Henry Ni mimi Jason.Nimepata ujumbe wako.”
            “Ndiyo Dr Jason nimekupigia nikakuta uko katika upasuaji .Dr Jason nakuomba uache shughuli zote hapo Dodoma na urejee mara moja hapa Dar es salaam. Leo Mzee Albano amerudishwa kutoka India hivyo Serikali ikatukabidhi sisi jukumu la kuhakikisha tunampatia huduma zote muhimu za kitabibu.Hapa tunapoongea niko na familia yake.Ninachoomba ni kwamba itatumwa ndege yetu leo saa kumi na mbili jioni ije ikuchukue ili uongoze jopo la madaktari katika matibabu ya mzee Albano”
            “Ok ! Dr Henry hakuna tatizo.Nitakuwa tayari muda huo ndege itakapofika” akasema Dr Jason
            “ Ok ! Dr Jason.See you then.Bye” Akakata simu na kuendelea na maongezi na familia ya mzee Albano.
******************************** 
            Saa kumi na mbili za jioni ndege ndogo  inayomilikiwa na hospitali ya Patrick Charles  memorial  ilitua katika uwanja mdogo wa hospitali hiyo uliopo pembezoni mwa majengo ya hospitali.Ni ndege iliyomleta Dr Jason bingwa wa neva za fahamu za ubongo na uti wa mgongo.Ni mmoja kati ya madaktari bingwa wachache sana wenye uwezo wa kipekee kabisa katika fani hii kwa ukanda huu wa Afrika.
            Dr Jason akapokelewa na Daktari mkuu Dr Henry kisha kwa mwendo wa kasi wakaanza kuelekea hospitalini.
            “Mgonjwa anaendeleaje? Akauliza Dr Jason
            “mgonjwa hali yake bado si nzuri.Mpaka sasa hivi bado hajarejewa na fahamu” Akasema Dr Henry
            Moja kwa moja wakaelekea katika chumba cha wagonjwa mahututi alimolazwa Mzee Albano. Alipoingia Dr Jason mle ndani ya chumba cha mgonjwa kila mmoja aliyekuwemo alionyesha tabasamu la matumaini usoni.Hii ilionyesha ni jinsi gani walivyokuwa na imani na Dr Jason.Kwa haraka akapewa taarifa ya maendeleo ya mgonjwa,akaomba apewe na faili la mzee Albano,kisha akaelekea ofisini kwake.
            Ni saa tatu za usiku sasa,masaa matatu yameshapita tangu Dr Jason alipoanza kulipitia faili la Mzee Albano.Alilipitia kwa umakini mkubwa sana na alilirudia  mara ya pili na ya tatu.aliporidhika akainua simu na kumpigia Dr Henry ambaye hakupoteza muda akafika ofisini kwa Dr Jason.
            “Dr Henry nimelipitia kwa makini faili la mgonjwa, kuna hivi vipimo nimeviorodhesha hapa ninataka vichukuliwe mara moja.Ni vipimo muhimu sana ambavyo vitatusaidia kuona jinsi ya kuanza kumsadia mgonjwa”
            Dr Henry akaichukua karatasi ile yenye vipimo alivyoviorodhesha Dr Jason akaiangalia kisha akasema.
            “Ok ! Dokta nafikiri timu nzima ya vipimo ipo tayari,ngoja watuletee vipimo hivyo”akatoka na kumwacha Dr Jason bado akiendelea kulipitia faili lile.
            Saa moja baadae Dr Henry alirudi akiwa na faili lenye vipimo vyote alivyovihitaji Dr Jason.
            “Kila kitu kiko humu Dr Jason.Kama kuna kitu kingine unahitaji niko ofisini”
            Jason akaliweka faili alilokuwa akilipitia  pembeni kisha akaanza kulipitia lile faili lenye vipimo alivyokuwa akivihitaji.Dakika zaidi ya arobaini alizitumia kuyapitia majibu yale ya vipimo alivyovitaka.Akasimama na kuzunguka humo chumbani huku akiangalia juu.Ni wazi kuna kitu kikubwa alichokuwa akikifikiria.Mwishowe akaamua kumwita Dr Henry.
            “Dr Henry nimepitia kwa umakini faili la mgonjwa na baadae majibu ya vipimo tulivyovifanya ”
            “yes Dr.” Akajibu Dr Henry kwa shauku ya kutaka kujua nini alichoitiwa
            “Dr Henry  kuna kitu nimekigundua katika uchunguzi wangu ambacho hawa wenzetu kule India walishindwa kukigundua.Pamoja na kwamba mabingwa wenzangu huko India walisema haiwezekani kwa mgonjwa kufanyiwa upasuaji lakini bado sijakubaliana nao kutokana na majibu ya vipimo nilivyovitaka.Nina kila sababu ya kukwambia kuwa tunaweza kumfanyia mgonjwa upasuaji  na kuokoa maisha ya mgonjwa.”
            Dr Henry alibaki mdomo wazi akiwa hana la kuongea.Alimuamini Dr Jason kupita kiasi kwani ni mmoja kati ya madaktari wenye uwezo na akili ya ajabu sana.Lakini kwa hili alionyesha mstuko wa dhahiri.
            “Najua umestuka sana Dr Henry baada ya kusikia kwamba ninaweza kumfanyia mgonjwa upasuaji ambao huko India wameshindwa.Siwewe tu ambaye anaweza kustushwa na jambo hili bali kila mtu anaweza akastuka akisikia kauli yangu,lakini ukweli ni kwamba mgonjwa bado anayo nafasi ya kuishi iwapo nitamfanyia upasuaji wa haraka.Nashindwa kuelewa kwa nini hawa madaktari wa India walishindwa kuligundua hili na kusema kuwa mzee huyu hawezi pona.Jambo hili linanipa wasi wasi mkubwa sana kama walifanya uchunguzi wa kutosha” akasema Dr Jason
            Saa nzima ilitumika kwa Dr Jason kumwelezea na kumfafanulia Dr Henry juu ya kile alichokigundua katika majibu ya vipimo na sababu ya kutaka upasuaji ule ufanyike.Dr Henry bado hakuwa na uamuzi hivyo akaamuru kuitishwa kikao cha dharura usiku huo cha madaktari pamoja na uongozi wa hospitali ili kuona kama kuna ulazima wowote wa kufanya operesheni hiyo.
            Haraka haraka ujumbe ukasambazwa kwa timu yote ya madaktari na kwa muda wa dakika ishirini  wote wakawa wamekusanyika katika chumba cha mikutano.Mkutano huu ulichukua zaidi ya masaa manne ndipo wote waliporidhika kuwa kweli kuna ulazima wa mzee Albano kufanyiwa upasuaji katika ubongo wake baada ya kuhakikishiwa na Dr Jason kwamba iwapo angefanyiwa upasuaji kulikuwa na uwezekano mkubwa wa kuyaokoa maisha yake..
            Ilipata saa tisa za usiku wakati Dr Henry alipompigia simu mke wa mzee Albano na kumtaka yeye na familia yake wafike hospitali hapo asubuhi na mapema kuna jambo la muhimu wanataka kuelezwa.  
  
*******************************  

            Ni milio ya ndege wa aina mbali mbali walioruka katika miti na bustani nzuri za maua zilizopo ndani ya jumba hili la kifahari ndizo zilizokuwa zimetawala.Ukimya mkuu ulikuwemo ndani ya jumba hili.Katika ghorofa ya juu kabisa kikao kizito kilikuwa kikiendelea . Mzee Bryson kamutere,mzee mwenye utajiri wa kutisha nchini Tanzania  alikuwa ndiye mwenyekiti wa kikao hiki.Pembeni yake alikuwepo binti yake ,mbunge mwenye umri mdogo kuliko wote katika bunge la jamhuri ya muungano wa Tanzania Stella kamutere,halafu wakawepo na watu wengine tisa wenye nyadhifa mbali mbali serikalini na mashirika binafsi.Alikuwepo Kumzaya ( Wakili wa kujitegemea na mfanyabiashara) , Ambakisye mwalukosa ( waziri wa kilimo ) ,Benard kukoa (mfanyakazi benki kuu ) , Nestory kazima ( mfanyakazi wizara ya fedha ) , Ernest kobwa ( Naibu waziri wa fedha ) , Sospeter Aloswa ( waziri wa maliasili ) , Azim Patel ( mfanyabiashara ) , Godwin Masawe ( mfanyabiashara) , Jacob simala ( mfanyakazi hazina) , Emmanuel Vincent ( afisa uwanja wa ndege) , Sixmund kamita (kamishna wa madini)
            “Ndugu wajumbe wa kikao hiki,nawashukuruni sana kwa kuitikia wito huu wa dharura  japo si wote mliohudhuria lakini mliopo mnatosha sana kuendesha kikao hiki.”
            Alifungua kikao Mr Kamutere.
            “Jambo tunaloenda kulizungumza ndugu zangu ni jambo zito.nafikiri wote mnazo taarifa za kurejeshwa nchini Mzee Albano.Mpango wetu ulikwenda vizuri sana kule India,madaktari katika hospitali ile aliyokuwa anatibiwa  walifanya kama vile tulivyowataka wafanye .Nilikuapo kule na niliongea nao wakanielewa na kukataa kumfanyia upasuaji mzee Albano na kuifanya familia yake kuamini kwamba mzee wao hawezi kupona hata kama akifanyiwa upasiaji.Haikuwa kazi ndogo kuwashawishi wale madaktari japokuwa imetugharimu fedha nyingi sana.Kwa sasa dunia nzima inaelewa kuwa mzee Albano hawezi kupona na hana siku nyingi za kuishi.Kwa muda wa wiki moja toka sasa mzee Albano atakuwa amekwisha fariki na  hilo ndilo hasa lengo letu.
            “ kwa nini hukuacha afanyiwe upasuaji na afariki wakati akifanyiwa upasuaji huko India?  Hakuna ambaye angehisi chochote kwani wagonjwa wengi tu hufariki wakati wakifanyiwa upasuaji”  akauliza Sixmund kamita
            “Hatukutaka afe kifo chenye mashaka.Tunataka kila mtu afahamu kwamba Albano alifariki kwa ugonjwa.Kurudi kwa Albano kusubiri kifo chake ni ushindi mkubwa  kwani alikuwa mtu hatari sana kwetu .Hatakiwi kabisa kuendelea kuvuta hewa hii safi.Pamoja na juhudi hizo za kuhakikisha kwamba mzee Albano haponi limeibuka tatizo dogo.Kwa mujibu wa vyanzo vyetu vya  uhakika toka hospitali ya Patrick Charles Memorial ambako Albano amelazwa baada ya kurudishwa toka India ni kwamba hivi tunavyoongea ,madaktari na familia ya Mzee Albano wako katika kikao.Kuna uwezekano mkubwa mzee Albano akaendelea kuwa hai kwa sababu kuna huyu daktari bingwa wa neva za fahamu za ubongo na uti wa mgongo anaitwa Jason Charles ambaye anataka kumfanyia upasuaji mzee Albano  na kuna uwezekano mkubwa  kuwa iwapo atafanyiwa upasuaji huu kuna uwezekano mkubwa sana Albano akapona.Daktari huyu inasemekana ni mmoja kati ya madaktari wachache wa  kutumainiwa katika masuala ya ubongo na uti wa mgongo si hapa Tanzania tu bali ukanda wote wa afrika mashariki na kati.Tunachotakiwa kukifanya kwa sasa ni kuhakikisha hilo halitokei kwa gharama zozote zile.Lazima tuhakikishe kwamba huyo daktari hafanikiwi kumfanyia upasuaji Albano.Tukikubali upasuaji huo ukafanyika na Albano akapona,siwafichi ndugu zangu lazima Albano atulipue kwani suala hili alikwisha liweka wazi ”Mzee Bryson akatulia akavuta pumzi na kuwaangalia wajumbe ambao pamoja na kuwa chumba walichokuwamo kuwa na kiyoyozi lakini bado nyuso zao zilionyesha kuvuja jasho.
            “Baba umesema Dr Jason Patrick Charles ndiye anayetaka kufanya huu upasuaji?” Stella akauliza kwa msisitizo huku akimtolea baba yake macho ya shauku
            “Yes my dear.Ni huyu huyu mchumba wako Dr Jason”
            " Unbeliavable !! akasema Stella.Hakuamini alichokisikia toka kwa baba yake.
            " Jason ndiye anayemfanyia upasuaji mzee Albano ! Ouh Mungu wangu lazima nimtaarifu aachane mara moja na mpango huo..they are going to kill him.Siwezi kukubali katu jambo hilo litokee.I love him so much " akawaza Stella.Hali yake ilibadilika ghafla baada ya kulisikia jina la mchumba wake likitajwa katika kikao kile.Hakuwa na amani tena 
**********************************            
            Dr jason aliwasili hospitali asubuhi na moja kwa moja akaelekea katika chumba maalum alicholazwa mzee Albano.Hali yake haikuwa na mabadiliko yoyote.Akatoka na kuelekea ofisini kwake kabla ya  kukutana na familia ya mzee albano ili kuielezea kwa ufasaha juu ya uamuzi wake wa kumfanyia operesheni baba yao.
            Siku hii alionekana mwingi wa mawazo na  hakutaka kujishugulisha na kazi nyingine yeyote licha ya kuwa  mafaili kadhaa ya wagonjwa hapo mezani kwake.Akili yake aliielekeza katika kitu kimoja tu,ugonjwa wa mzee Albano.Akiwa bado katika mawazo mengi mara simu yake ikaita  alikuwa ni Daktari mkuu Dr Henry.
            “Dr Henry habari za asubuhi.’
            “Nzuri Dr Jason.habari za toka jana?”
            “Nzuri tu .Mimi tayari nimeshafika ofisini ,nimetoka kumuangalia mgonjwa hali yake haina mabadiliko yoyote.”
            “ Dr Jason nadhani ni wakati sasa wa kukutana sasa na familia ya Mzee Albano pale katika chumba kidogo cha mikutano ili tuongelee suala hili la mzee wao, nilipata taarifa kuwa walikwisha fika muda mrefu sana na nikaelekeza wapelekwe kule ili tukaongee nao.”
            “Ok ! Dr Henry nakuja sasa hivi” Akajibu Dr Jason na kukata simu kisha akatoka na kuelekea katika chumba kidogo cha mikutano.
Muda mchache baadae tayari alikwisha fika,akakinyonga kitasa na kuingia ndani.Chumba kilikuwa na madaktari pamoja na familia yam zee Albano.Ghafla Dr Jason akasimama.Alikiona kitu ambacho hakutegemea kukiona.
            “Serenaa…!!!!!!.  Akasema Dr Jason kwa mstuko  mkubwa.
 Kila mtu mle chumbani akastuka na kubaki akishangaa.Serena ambaye alikuwa ameongozana na mama yake na Isabella naye akabaki ameduwaa akishangaa.
            “ Jason ..!!!!!  ..akasema Serena kwa sauti ndogo.Isabella mdogo wake aliyekuwa amekaa pembeni yake akageuka na kumtazama dada yake kwa mshangao.


0 comments:

Post a Comment

Followers

 

BONYEZA "LIKE" NA UJIUNGE NASI MOJA KWA MOJA KWA SIMULIZI MPYA KILA SIKU

Powered By masimulizi